Sunday, September 9, 2012

Mcheza filamu mkali wa hapa Bongo  Jacqueline Wolper hivi karibuni alimshtua mama’ake mzazi, wakiwemo wadau wa filamu baada ya kuonekana amelazwa katika machela  akiwa hoi taabani.
Tukio hilo ambalo lilikusanya watu wengi lilijiri Kibaha Mkoa wa Pwani ambako pia ndiko anakoishi mama mzazi wa staa huyo.
Watu  waliomzunguka yeye akiwa kitandani walisababisha waliokuwa wakipita kufika eneo hilo kutaka kujua kulikoni, wengine walikwenda kumwambia mama yake kuwa binti yake ameugua ghafla na kumfanya mwanamke huyo kuchanganyikiwa.
Habari zikaendelea kudai kuwa, kufuatia hali hiyo, Mama Wolper alimpigia simu mwanae kumuulizia kuhusu alichosikia, lakini akamjibu haumwi yupo kazini.
Kwenye eneo la tukio, wakati watu wakiendelea kuulizana ndipo ilipogundulika kuwa staa huyo alikuwa akirekodi filamu.
Baadhi ya watu walionekana wakicheka baada ya kugundua kumbe kilichokuwa kikiendelea ni filamu na si tukio halisi.  
“Yaani mimi niliogopa, nilijua labda amepata matatizo au anaumwa ameletwa kwa mganga wa kienyeji,“ alisikika mtu mmoja akiwaambia wenzake huku wakitawanyika eneo la tukio.
Wolper alipopigiwa simu juzi Alhamisi, alikiri kulala kwenye kitanda cha kamba akiwa anarekodi filamu na si kwamba alikuwa mgonjwa.

0 comments:

Post a Comment