TCU: Vyuo vijisajili Nacte


TUME ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), imeviagiza vyuo  vinavyotoa mafunzo kwa ngazi ya stashahada nchini kuhakikisha vinatambuliwa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (Nacte).
Akizungumza na waandishi wa habari jana kuhusu maonyesho ya Vyuo Vikuu yatakayoanza leo Jijini Dar es Salaam, Naibu Katibu Mtendaji wa TCU, Profesa Magishi Mgasa alisema kuwa haiwezekani vyuo visivyotambuliwa na Nacte kuendelea kuwepo nchini.

“Tumevitaka vyuo vinavyoendelea kutoa mafunzo kwa wananchi huku vikiwa havitambuliwi na Nacte, kuhakikisha vinasajiliwa ili kuepuka usumbufu wanaoupata walengwa wanapohitimu katika vyuo hivyo,” alisema Profesa Mgasa.

Alisema kwaba hatua hiyo ina lengo la kuondoa usumbufu kwa wanaomaliza vyuo hivyo hasa wanapotaka kudahiliwa katika vyuo vya elimu ya juu kupitia TCU ambayo sasa haiwatambui.

“Mwanafunzi hatakuwa na sifa za kudahiliwa kupitia njia ya TCU ikiwa chuo anachosoma hakitambuliwi na TCU. Hivyo ili kuepuka usumbufu huo ni lazima wahusika wakachukue hatua zaidi,” alisema Profesa Mgasa.
Kuhusu maonyesho hayo Profesa Mgasa alisema kuwa yatatoa nafasi kwa wanafunzi wanaotarajiwa kujiunga na elimu ya juu kujua ubora wa vyuo mbalimbali kabla ya kujiunga.

“Vyuo shiriki vitakuwa zaidi ya 65 vya ndani na nje ya nchi, hivyo wananchi na wanafunzi watapata nafasi ya kuelewa mambo mbalimbali yanayotolewa na chuo shiriki,” alisema Profesa Mgasa na kuongeza:
Tofauti na vyuo vitakavyoshiriki pia kutakuwepo na taasisi mbalimbali zinazohusika na masuala ya utafti zikielezea tafti ambazo wamezifanya na hatua zilizofikiwa mpaka sasa hapa nchini.

Alisema kuwa mwaka huu TCU imepanua wigo wa udahili kwa wanafunzi kujiunga na elimu ya juu tofauti na awali ambapo iliwatambua wanaotoka shule moja kwa moja pekee.

“Hapo awali njia yetu ya udahili ilikuwa inawahusisha wanafunzi waliomaliza kidato cha sita moja kwa moja lakini sasa wanaomaliza Stashahada kutoka vyuo vinavyotambuliwa na Nacte nao wanakubaliwa,” alisema Profesa Mgasa na kuongeza:

Kwa wanafunzi waliohitimu Stashahada katika vyuo visivyotambuliwa na Nacte wao hawatakuwa na sifa za kudahiliwa na TCU ila watatakiwa kuomba moja kwa moja vyuoni.

Maonyesho hayo yameandaliwa na TCU na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi yanatarajiwa kufungiliwa leo na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Mohammed Gharib Bila na kufikia kilele chake kesho kutwa.

0 comments:

Post a Comment