Saturday, June 23, 2012

na Charles Misango, Dodoma
SIKU moja baada ya Mbunge wa Musoma Vijini, Nimrod Mkono (CCM), kuibu ufisadi mpya katika mgodi wa makaa ya mawe Kiwira, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amezima hoja hiyo akidai mbunge huyo ana maslahi ya kibiashara.

Profesa Muhongo, alitoa kauli hiyo jana wakati akijibu hoja za wabunge katika kuhitimisha mjadala wa taarifa ya hali ya uchumi na mpango wa maendeleo kwa miaka mitano, iliyowasilishwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wassira.
Akizungumza kwa kujiamini, waziri huyo bila kumtaja Mkono kwa jina, alisema kuwa hawezi kujibu hoja zake kuhusu ufisadi wa Kiwira kwa vile mbunge huyo ni mwakilishi wa kampuni moja ya Dubai ya madini, na hivyo asingeweza kuzungumzia taarifa za watu walio katika ushindani wa kibiashara.

Hata hivyo, hoja hiyo ilionekana kumkera Mkono, ambaye aliomba kutoa taarifa na kumtaka waziri huyo kufuta kauli yake kwa vile katika mchango wake wa kimaandishi, aliweka bayana kuwa ana mgongano wa kimaslahi kama kanuni zinavyotaka.
“Mheshimiwa Spika, jana wakati nachangia niliweka wazi mgongano wa kimaslahi, ingawa nilifanya hivyo kimaandishi kutokana na muda mdogo wa kuchangia kwa maneno. Hivyo namwomba waziri kufuta kauli hiyo,” alisema Mkono.

Ombi lake nalo liligonga mwamba baada ya Spika Anne Makinda, kudai kuwa, hata waziri hakuwa amemtaja jina hivyo si lazima kulalamikia jambo hilo.
Mkono ambaye alilazimika kutii amri ya kiti, alionekana kuzungumza chini chini, kabla ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA) kusimama na kuomba mwongozo, akitaka waziri ajibu hoja za tuhuma za Kiwira hata kama hakutaka kujadili suala la uhusiano wa maslahi wa mbunge Mkono, kwa vile ni nzito na zinahitaji majibu yakinifu.

Hoja ya Mnyika nayo ilipigwa chini na Spika kwa kudai kuwa, suala hilo litamalizwa kwa kufuata utaratibu.
Juzi, wakati akichangia mjadala wa hotuba ya bajeti ya serikali kwa mwaka 2012/2013, Mkono alidai kuwa uuzaji wa mgodi huo ni kinyume na makubaliano yaliyofikiwa na Bunge mwaka 2007 ambapo liliagiza kwamba mgodi huo uliokuwa umeuzwa kwa Kampuni ya Tan Power urudishwe serikalini baada ya kuwa umeuzwa kwa dola laki saba tu.

Mkono alisema kuwa katika hali ya kushangaza, Kampuni ya Tan Power ambayo ilikuwa imeingia ubia na serikali iliuzwa kwa Waustralia kiasi cha mabilioni ya dola.
Aliliomba Bunge kuunda kamati maalumu kuchunguza uuzaji wa Kampuni ya Tan Power kwa bei ya kutupwa kwa kampuni moja ya Australia.

“Mheshimiwa Spika, Kiwira kulikoni? Lini Bunge litaunda kamati ya kwenda kuangalia Kiwira?” aliuliza mbunge Mkono ambaye pia ni mwanasheria maarufu nchini.
Alisema pamoja na yote hayo, sasa serikali imetenga sh bilioni 40 kwa ajili ya mradi wa Kiwira na kuhoji nani aliteketeza fedha za awali zilizotolewa kwa ajili hiyo.
Katika hatua nyingine, Waziri Muhongo alitangaza kiama kwa wafanyakazi wa Shirika la Ugavi wa Umeme nchini (TANESCO) na kuagiza kuwa kuanzia sasa atawawajibisha mara moja watendaji watakaofanya kazi kwa uzembe.

Aliagiza shirika hilo kuhakikisha limewawekea umeme wateja wote walioomba na kulipia kufikia Juni 31.
“Natoa amri kuwa wale wote waliokuwa wamelipia kabla ya 31 Mei, wanapaswa kuunganishiwa umeme mwisho wa mwezi huu na ikiwa bado watoe taarifa wizarani ama kwangu mwenyewe.
“Mambo sasa ni kwa vitendo, na TANESCO wajue kuwa hakuna mjadala katika utendaji wa kazi. Ama wanatekeleza au hawawezi,” alisema.

Kuhusu gesi, alisema rasimu ya sera ya gesi itapitiwa na wataalamu wote Julai, na kisha wataitisha maoni ya Watanzania nchi nzima ili waichambue, na watakwenda katika mikoa ya Lindi na Mtwara kuwashirikisha wananchi wa huko kabla ya kuleta muswada bungeni Oktoba mwaka huu.
Kwa upande wa madini, alisema kuwa leo atakutana na wachimba madini kote nchini ili kuweka mikakati ya namna ya kuboresha uchimbaji na ukusanyaji kodi na umiliki wa leseni.

0 comments:

Post a Comment