Saturday, June 16, 2012

KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, ameiponda hotuba ya bajeti iliyosomwa bungeni juzi, akisema inaonyesha wazi kuwa serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM), imefikia mwisho wa kufikiri.
Alisema kuwa kitendo cha serikali kushindwa kutafuta vyanzo vipya vya mapato na badala yake kuendelea kutegemea vinywaji laini na vileo na kuruhusu wananchi waweke majina yao kwenye pleti za magari badala ya namba za magari ni hatua kuwa hawana ubunifu wa kukuza uchumi.

Akizungumza na Tanzania Daima jana jioni kwa njia ya simu kuhusu bajeti hiyo, Dk. Slaa ambaye alikuwa mbunge wa Karatu kwa vipindi vitatu mfululizo, alisema licha ya kwamba ni mapema kutoa maoni lakini bajeti imejaa matamko ya kisiasa.
“Hayo aliyosoma Waziri William Mgimwa ni matamko ya kisiasa si hotuba ya bajeti, kwani tunaoelewa bajeti ni vitabu vinne wanavyopewa wabunge, nami navingojea nimeomba nipatiwe ila kama ndiyo hivyo alivyosoma tuko kwenye hali mbaya,” alisema Dk. Slaa.
Alisema kuwa kinachoshangaza ni kuongezeka kwa deni la taifa halafu fedha zinazokopwa na serikali imezielekeza kwenye matumizi ya kawaida badala ya maendeleo.

“Taifa linakopa ili iweje, kulipana mishahara na posho ama? Hii ni hatari kwa vizazi vijavyo miaka 30 hadi 40 ijayo. Zamani hata serikali zilizotangulia zilikopa lakini mikopo hiyo ilitumika kujenga viwanda, shule, barabara na huduma nyingine, leo tunafanya hivyo?” alhoji.
Alisema inashangaza kuona serikali inakopa kutoka vyombo vya biashara halafu inapelekea fedha hizo kwenye uendeshaji jambo lililozifanya hata taasisi za fedha za kimataifa kuwanyima mikopo na hivyo wamekimbilia kwenye mabenki.
Alifafanua kuwa ni katika makosa kama hayo imenyimwa mkpo wa sh bilioni 480 kwa ajili ya Shirika la 

Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO).
Kuhusu vyanzo vya mapato, Dk. Slaa alisema anashangaa kuona kila mwaka serikali akili yake inalalia kuongeza kodi kwenye vileo na kuacha sekta nyeti kama madini.
“Tumerudia vyanzo vile vile ukiacha hicho cha watu kuruhusiwa kutumia magari yenye majina yao badala ya namba za usajili, sasa labda walevi watakapogoma kunywa ndipo serikali itapata ubunifu wa kuangalia vyanzo vingine,” alisema.

Hata hivyo, Dk. Slaa aliponda chanzo kipya cha mapato cha kuwaruhusu watu kuweka majina badala ya namba, akidai kuwa hatua hiyo mbali na kuleta matabaka kisaikolojia kwa wenye fedha kujiona wameiweka serikali mfukoni lakini pia ina madhara kuichumi.
“Mafisadi hawaoni uchungu hata kidogo kutumia fedha ila jambo la msingi ni kwamba wamezipataje, sasa kwa hali kama hii watafurahi kwa vile wanaona serikali imewahalalisha bila kujali kama fedha zao ni haramu,” alidai.
Aliongeza kuwa hata, vipaumbele ambavyo serikali imeelekeza kwenye bajeti yake, utekelezaji wake utakuwa mgumu kwani fedha zilizotengwa ni ndogo ikilinganishwa na mahitaji halisi.habari na http://www.freemedia.co.tz/daima

0 comments:

Post a Comment