Saturday, June 16, 2012

WAZIRI wa Fedha na Uchumi, Dk. William Mgimwa, anadaiwa kusoma hotuba ya bajeti iliyojaa kasoro nyingi, ikiwa ni pamoja na kukosekana kwa vipengele muhimu vilivyokubaliwa na Kamati ya Uchumi na Fedha.
Kwa kufanya hivyo, waziri huyo sasa anashutumiwa kwa kuidharau na kukiuka kwa makusudi maagizo ya kamati hiyo yaliyokuwa na lengo la kuiboresha bajeti ili ilete manufaa kwa wananchi.
Tuhuma hizo nzito zilitolewa jana na mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM), mbele ya waandishi wa habari, na kutangaza rasmi kuipinga bajeti hiyo kwa madai kuwa haina tija kwa wananchi wanyonge.
Aidha alisema kuwa bajeti iliyosomwa bungeni ilikataliwa na kamati hiyo bungeni kutokana na kubaini kuwa ni mbovu na haikidhi vigezo na malengo ya kumkomboa Mtanzania maskini.
Mpina ambaye ni mjumbe wa kamati hiyo, alisema kuwa walimtaka Waziri Mgimwa kwenda kuifumua upya na kufanya marekebisho, lakini serikali imekataa ikitoa sababu na visingizo vingi.
Kwa kujiamini, Mpina alisema kitendo cha waziri Mgimwa kutojali mapendekezo yao, kimeifanya bajeti hiyo kuonyesha kuwa serikali haina nia njema ya kuboresha maisha ya Watanzania ambao kila siku wanapiga kelele juu ya kuwepo kwa umaskini uliokithiri.
Mpina alisema kuwa anajua msimamo wake huo, unaweza kumletea matata ndani ya CCM, lakini akadai kuwa yuko tayari kwa lolote hata ikiwa ni kufukuzwa ndani ya chama hicho.
Mpina alisema bajeti hiyo imejaa upungufu mwingi, ikiwemo kuelekeza fedha nyingi katika matumizi makubwa ambayo siyo ya msingi na kuyaacha mambo ya maendeleo.
Alifichua kuwa bajeti hiyo, pia imekiuka makubaliano ya wabunge ya utekelezaji wa mpango wa miaka mitano wa maendeleo ambao unalenga kuboresha maisha ya Watanzania ambao wamekata tamaa kutokana na umaskini walionao.
Mpina alibainisha kasoro nyingine kubwa kuwa ni ukiukwaji wa maagizo ya wabunge ambao waliitaka serikali kuhakikisha kila mwaka wa fedha inatenga sh tirilioni 2.7 kutoka katika fedha za ndani kugharamia miradi ya maendeleo na kutenga asilimia nyingine 35 ya bajeti kwa ajili hiyo.
Mbunge huyo alisema pia katika makubaliano ya wabunge na serikali yaliyokiukwa katika bajeti hiyo ni kuhakikisha kuwa fedha za umma zilizotengwa kwa ajili ya shughuli za maendeleo hazitumiki kwa ajili ya mambo mengine.
Mpina alizidi kufichua kuwa wakati wa kujadili mpango wa maendeleo wa miaka mitano, aliyekuwa Waziri wa Fedha Mustafa Mkulo, aliwahakikishia wabunge kuwa mambo hayo yangezingatiwa kikamilifu na fedha hizo zingetengwa kila mwaka, ikianza na bajeti ya mwaka huu.
“Lakini ukisoma bajeti iliyowasilishwa na Waziri wa Fedha na Uchumi inaonesha kuwa matumizi ya kawaida yametengewa trilioni 10.5, sawa na asilimia 70, na matumizi ya maendeleo yametengewa trilioni 4.5, sawa na asilimia 30, wakati fedha za ndani zilizotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ni trilioni 2.2 tu, badala ya 2.7,” alisema.
Alisema kitendo cha serikali kutenga trilioni 2.2 badala ya trilioni 2.7 ambayo inaleta tofauti ya sh bilioni 500, iliyoainishwa awali katika mpango wa maendeleo, kimeifanya miradi mingi kutengewa fedha kidogo huku mingine mingi ikikosa fedha kabisa.
“Kibaya zaidi katika bajeti hii, mapato ya ndani kwa sasa yameongezeka kwa trilioni 1.5, huku matumizi ya kawaida yakipanda kwa trilioni 1.9 wakati fedha za maendeleo zikipungua kwa bilioni 397.8 ikilinganishwa na mwaka wa fedha 2011/12.
“Hapa inadhihirisha dhahiri kuwa serikali haina nia ya dhati ya kupunguza matumizi ya kawaida,” alisema Mpina.

Mbunge huyo alizidi kusisitiza kuwa wakati serikali ikiendeleza matumizi makubwa yasiyokuwa na tija, Watanzania wengi wanakufa kwa kukosa matibabu kutokana na kukosekana kwa zahanati, dawa na waganga na wengine wakikabiliwa na ukosefu wa maji safi na salama, elimu bora kutokana na upungufu mkubwa wa madarasa na nyumba za walimu.

Mpina aliongeza kuwa kwa kipindi kirefu serikali imekuwa ikitoa ahadi za kupunguza matumizi ya kawaida ili kuongeza kasi ya utoaji huduma na uwekezaji katika sekta zinazokuza uchumi na kupunguza umaskini.
Alitoa mfano wa wizara mbili za Nishati na Madini na Fedha na Uchumi ambazo zimejipangia kiasi kikubwa cha fedha kwa matumizi aliyoyaita kuwa si ya lazima.
Kwa Wizara ya Nishati na Madini, Mpina alibainisha kuwa imejitengea sh milioni 142 kwa mwaka huu wa fedha kwa ajili ya mafunzo ya nje, wakati mwaka jana ilitenga sh milioni 34, hivyo kuwa na ongezeko la milioni 108.

Wizara hiyo itatumia sh milioni 567 kwa ajili ya mawasiliano, badala ya milioni 71.76 ilizotumia katika mwaka wa fedha 2011/12, wakati katika kile kilichoitwa Kitengo cha Utawala na Mawasiliano kitatumia sh bilioni 2.003 badala ya sh milioni 53.87 za mwaka jana.
Nayo Wizara ya Fedha na Uchumi imejitengea sh milioni 582.3 kwa safari za wakubwa za ndani, katika Idara ya Utawala na Rasilimali Watu, wakati mwaka jana ilitumia sh milioni 283, na safari za nje itatumia sh milioni 874,wakati mwaka jana ilitumia sh milioni 532.Habari na http://www.freemedia.co.tz/daim

0 comments:

Post a Comment