Monday, June 18, 2012

KWA mara nyingine tasnia ya habari nchini imepata pigo la kuondokewa na Mhariri Mkuu wa gazeti la kila siku la Jambo Leo, Willy Edward (38), aliyefariki ghafla usiku wa kuamkia jana akiwa mjini Morogoro.
Willy pamoja na wahariri wenzake wa vyombo mbalimbali vya habari, walikuwa mkoani humo, kuhudhuria semina ya siku moja iliyoandaliwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), kuhusu sensa ya watu na makazi.

Taarifa za kifo chake zilitolewa na mhariri mwenzake wa gazeti la Mtanzania, Kulwa Karedia, ambaye alikuwa naye kabla ya kufikwa umauti, akisema kuwa alikuwa ni mzima wa afya, na kwamba aliwaaga anakwenda kuwaona watoto wake ambapo alikaa huko mpaka saa 6:30 usiku.
Alisema muda wa kurudi hotelini alikokuwa amefikia ulipofika, Willy alimwita dereva wa pikipiki ili amchukue, lakini usafiri huo ulipofika hakuweza kuupanda kwani alipotoka nje na kutembea kwa hatua chache alianguka.
Karedia aliongeza kuwa, ndugu zake walimkimbiza hospitalini na baada ya vipimo vya daktari, ikabainika kuwa alikwishafariki dunia.
Kaka wa marehemu azungumza
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, kaka wa marehemu, Denis Ongiri, alisema wanatarajia kuzika mjini Mugumu wilayani Serengeti, Mara.
Alisema kwa sasa msiba upo nyumbani kwa kaka yao eneo la Mburahati NHC na kwamba taratibu za kusafirisha mwili kwa ajili ya mazishi zitatolewa baada ya ndugu kukutana na kutoa uamuzi wa pamoja.
“Suala hili limekuwa la ghafla sana, ninachoweza kusema kwa sasa ni kwamba tutaenda kumzika wilayani Serengeti katika mji wa Mugumu, tunaomba ushirikiano wa watu wote katika hili kuanzia sasa mpaka safari yake ya mwisho,” alisema Ongiri.
Mwili wa marehemu Willy, ulihamishwa toka Hospitali ya Mkoa Morogoro jana na kupelekwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar es Salaam ambako utahifadhiwa.
Gari lililobeba mwili huo, liliwasili Muhimbili jana majira ya saa 11 jioni likiwa na wanafamilia na wanahabari kadhaa kisha mwili kushushwa na kuingizwa chumba cha kuhifadhia maiti.
Wakati wa kupokea mwili huo, watu mbalimbali wakiwemo wanahabari, walishindwa kujizuia na hivyo kuangua vilio wasiamini kile walichokuwa wakikishuhudia.
Historia yake
Willy Edward Daniel Ogunde, alizaliwa Machi 7, 1974 katika Wilaya ya Serengeti mkoani Mara, na kusoma Shule ya Msingi Mapinduzi mwaka 1983-89. Elimu ya sekondari aliipata katika shule ya Serengeti mwaka 1990-93 na kuendelea na kidato cha tano na sita katika Shule ya Sekondari Musoma.
Mwaka 1996 alijiunga na kampuni ya uchapishaji wa magazeti ya Business Times Ltd (BTL) akiwa mwandishi wa gazeti likiitwa Majira Jioni wakati huo.
Akiwa na kampuni hiyo, alipata mafunzo mafupi ya kikazi yakiwemo ya kompyuta na ya uandishi wa habari.
Mwaka 1998 alihamishwa kitengo kutoka kwenye gazeti la Majira Jioni kwenda kwenye gazeti jipya la Dar Leo na kuwa mwandishi wa habari wa gazeti hilo, lakini pia akishikilia nafasi ambazo alikuwa akizitumikia kwenye gazeti la Majira Jioni.
Alifanikiwa kuaminika kutokana na uwezo wake kazini na hivyo alipanda daraja na kuwa mhariri wa gazeti la Dar Leo kuanzia mwaka 2002 hadi 2005.

Kipindi cha mwaka 2006 hadi 2007 alikuwa akitumikia nafasi ya mhariri msaidizi wa michezo wa gazeti la Majira na baadaye mwaka huo akawa mhariri wa michezo wa gazeti hilo.
Mwaka 2006 hadi 2007 alipata cheti cha elimu ya uandishi wa habari katika Chuo cha Ceylon (CSJ).
Amesafiri nchi mbalimbali duniani katika kuripoti habari za michezo na burudani, ikiwemo Afrika Kusini mwaka 2003 hadi 2006 kwenye mashindano ya Big Brother Africa.
Pia mwaka 2007, 2008 na 2009 alikwenda Kenya, Senegal na Uingereza kuripoti habari za michezo kupitia Super Sport.

Mei mwaka huu, alisafiri kwenda nchini Uturuki kwenye kongamano la wadau wa masuala ya mawasiliano, ambako alikuwa kiongozi wa wahariri waliotoka Tanzania na kutoa mada iliyohusu mwenendo wa vyombo vya habari nchini Tanzania.
Nje ya kazi ya uandishi wa habari, mwaka 2008 na 2009 alifanya kazi katika kampuni ya matangazo ya ZK akiwa Ofisa Habari na Uhusiano.
Miongoni mwa vyombo vya habari ambavyo aliwahi kufanya kazi enzi za uhai wake ni pamoja na kampuni ya New Habari ambayo aliitumikia mwaka 2007 na 2008 akiwa mhariri msaidizi wa gazeti la Bingwa.

Hatimaye mwaka 2008 alikuwa mhariri mkuu wa gazeti la Bingwa kabla hajaacha kazi katika kampuni hiyo na kujiunga na ZK.
Mwaka 2010 alijiunga na gazeti la Jambo Leo, akiwa mhariri wa habari na kuanzia mwaka jana hadi mauti yalipomkuta alikuwa mhariri mkuu wa gazeti hilo.
Marehemu ameacha mke na watoto watatu, mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahala pema peponi. Amina
 http://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=37099

0 comments:

Post a Comment