Sunday, May 27, 2012

TIMU za soka Tanzania ‘Kilimanjaro Stars’ na Malawi ‘The Flames’ jana zimeshindwa kutambiana baada ya kulazimisha sare ya bila kufungana katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki uliopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Mchezo huo ulikuwa ni mahususi kwa timu hizo kujinoa kwa ajili ya mechi zake za mchujo wa kuwania kucheza Kombe la Dunia Juni 2, ambapo Stars itakuwa Ivory Coast, huku Malawi itakwaana na Kenya ambapo zote zitacheza ugenini.
Katika mchezo wa jana timu timu hizo zilionekana kusomana zaidi ambapo wachezaji wake walijaribu kufanya mashambulizi ya hapa na pale lakini hayakuleta matunda yoyote.
Dakika ya 33 Joseph Kamwendo wa Malawi alikosa bao la wazi baada ya shuti lake kugonga mwamba.
Dakika ya 40 Kazimoto naye alishindwa kutikisa nyavu za Malawi baada ya shuti lake kupanguliwa na kipa, Simplex Nthala.
Mwamuzi wa kimataifa, Oden Mbaga, alimlima kadi ya njano Kamwendo katika dakika ya 43 baada ya kumchezea vibaya Kazimoto.
Malawi ilionekana kuishambulia zaidi Stars lakini jitihada za Kipa Juma Kaseja ziliwezesha kuzuia nyavu zake kutikiswa. Hivyo kipindi cha kwanza kumalizika kwa sare 0-0.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku kila timu ikionekana kuwa na uchu wa kupata bao ambapo katika harakati hizo mshambuliaji wa Stars Mbwana Samatta alikosa bao la wazi katika dakika ya 58 baada ya shuti lake kutoka nje.
Mbaga alimzawadia kadi ya njano nyota wa The Flames, James Sangala, baada ya kumchezea vibaya Samatta.
Katika mchezo huo Stars inayodhaminiwa na Kampuni ya bia Tanzania (TBL) kupitia bia yake ya Kilimanjaro ilimtoa Wazir Salum na kumuingiza Amir Maftah, huku The Flames ikiwatoa Dave Banda, Zicco Mkanda, Russell Mwafulirwa na kuwaingiza Jimmy Zakazaka, Amadu Ally na Ndaziona Chatsalira.
Katika mchezo ambao hadi dakika 90 zinamalizika hakuna timu iliyoweza kuliona lango la mwenzake, Kili Satrs inayonolewa na Mdenish Kim Poulsen, ambaye jana ilikuwa ni kibarua chake cha kwanza tangu arithi mikoba ya Mdenish mwenzake, Jan Poulsen, ilionekana na mabadiliko makubwa na hasa wachezaji wake kuonekana wamepikwa vema.
Hata hivyo chipukizi waliomo katika kikosi cha Stars kama Frank Domayo walionekana kutozoea mikiki, huku safu ya kiungo ikionekana kutowasiliana vema na washambuliaji, wakati nafasi ya ulinzi nayo kidogo ilionekana kuzubaa.
Stars: Juma Kaseja, Shomari Kapombe, Wazir Salum/Amir Maftah, Aggrey Morris, Kelvin Yondan, Shaban Nditi, Mrisho Ngasa, Frank Domayo, Mbwana Samatta, Haruna Moshi ‘Boban’ na Mwinyi Kazimoto.
Malawi: Simplex Nthala, Limbikani Mzava, Moses Mvula, Foster Namwela, James Sangala, Joseph Kamwendo, Frank Banda, Dave Banda/Jimmy Zakazaka, Zicco Mkanda/Amadu Ally, Robin Ngalande na Russell Mwafulirwa/ Ndaziona Chatsalira.

0 comments:

Post a Comment