Sunday, August 4, 2013

Tamko hili limetolewa leo tarehe 3 august 2013, mkoani mbeya katika ukumbi wa royal zambezi

KIKAO CHA WALIMU WA MKOA WA MBEYA CHA KUJADILI MASLAHI YA WALIMU WA TANZANIA-Tarehe 3 August, 2013.


1.     CHAMA CHA WALIMU-CWT NA WALIMU.
a.      Umuhimu wa chama cha walimu katika kufuatilia maslahi na madai mbalimbali ya walimu. CWT imeshindwa kuwasaidia walimu katika kufuatilia madai ya maslahi mbalimbali kama vile kupanda madaraja, malimbikizo ya mishahara, nauli n.k ambapo jukumu la chama sasa jukumu hili limekuwa likifanywa na walimu wenyewe alihali tukichangia chama kwa ajili ya kutetea walimu.
b.      Uwajibikaji wa Chama cha walimu-CWT kwa walimu. CWT imeshindwa:-
i.                    Kutoa, elimu, taarifa, mbalimbali kwa walimu hii ikiwemo katiba ya Chama Cha Walimu-CWT, Kanuni za kudumu utumishi wa umma kwa walimu  ili kutufanya tutambue vizuri haki na wajibu wetu kama watumishi.
ii.                  Kutoa taarifa kwa walimu juu ya mwenendo wa majadiliano kati ya serikali na CWT kuhusu madai ya nyongeza ya mishahara kwa 100%, posho ya mazingira magumu, posho ya kufundishia na posho ya walimu wa sayansi n.k. CWT imekaa kimya kwa muda sasa tangu mahakama isitishe mgomo wetu na kutuamuru turudi kazini huku mahakama ikiiamuru serikali kukaa meza moja na CWT ili kufikia muafaka. Umepita muda sasa chama cha Walimu-CWT hakijatoa taarifa yoyote kwa walimu kuhusu hatma ya madai hayo ya walimu. Hii inadhihirisha kuwa chama cha walimu aidha kimeamua kuwasaliti walimu kwa kushirikiana na serikali yaani mwajiri wetu.
c.       MCHANGO wa kila mwezi. Walimu wa mkoa wa Mbeya kwa niaba ya walimu wa Tanzania tunahoji uhalali wa chama cha walimu-CWT kukata fedha kila mwezi kama mchango wa chama alihali si wanachama wa Chama hicho.

2.     SERIKALI YA JAMHURI MUUNGANO WA TANZANIA NA WALIMU
Serikali ya jamhuri ya muungano wa Tanzania imekuwa ikifanya yafuatayo kwa kwa kada ya utumishi wa umma hasa ualimu:-
a.      Kuligawa Taifa kimakundi na kuvunja umoja wa kitaifa kwa kufanya yafuatayo:-
i.                    Kuweka tofauti kubwa ya kipato cha mshahara kwa wafanyakazi wa serikali wenye elimu sawa katika kada tofauti. Mfano kwa mujibu wa waraka wa watumishi wa serikali Na 1.  Wa mwaka 2013, wenye Kumb. Na. CAC.205/228/01/C/14 wa Julai 2, 2013 uliosainiwa na Katibu mkuu Utumishi Ndugu George D. Yambeshi. Unaoonyesha marekebisho ya mishahara kwa watumishi wa serikali. Katika waraka huu unaendelea kudidimiza kada ya ualimu kulingana na kada zingine kama vile kada ya afya, sheria na kilimo na utafiti ambapo kada hizi hulipwa mishahara mikubwa kuliko ya walimu. Kwa mujibu wa katiba ya jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 Toleo la mwaka 2005 ibara ya 23(1) inasema “Kila Mtu, bila ya kuwapo ubaguzi wa aina yoyote, anayo haki ya kupata ujira unaolingana na kazi yake, na watu wote wanaofanya kazi kulingana na uwezo wao watapata malipo kulingana na uwezo na kiasi kiasi na sifa za kazi wanazozifanya”. Je, serikali ya Jamhuri ya Muungano inatulipa walimu ikitofautisha mshahara huo na kada zingine kwa vigezo kwamba:-
a.      Uwezo wetu wa kufanya ya kazi haufanani na kada hizo?
b.      Umuhimu wa kada ya ualimu ni mdogo tofauti na kada hizo nyingine?
c.       Sifa za kielimu walizonazo walimu ni tofauti kabisa na kada hizo?
d.      Umuhimu wa walimu na elimu ni mdogo katika Jamhuri yetu ya Muungano wa Tanzania ukilinganisha na sekta kama vile Kilimo na Afya?
e.      Au hii ni mbinu ya “divide and rule” kwa wafanyakazi?
 NGAZI YA ELIMU
UALIMU/ ELIMU
KILIMO
AFYA
Certificate (Cheti)
Tsh 344,000/=
Tsh 1,060,000/=
Tsh 562,000/=
Diploma (Stashahada)
Tsh 432,500/=
Tsh 1,252,000/=
Tsh 821,000/=
Degree (Shahada)
Tsh 589,000/=
Tsh 1,473,000/=
Tsh 994,000/=
Jedwali hili ni kwa mujibu wa waraka huo uliotajwa hapo juu

b.      Kulubuni vyama vya wafanyakazi ikiwemo Chama cha Walimu-CWT ili kuacha majukumu yake ya kutetea na kutoa elimu juu ya haki na wajibu wa wafanyakazi ila vyama hivyo kushirikiana na serikali kukandamiza haki za wafanyakazi. Baadhi ya mbinu ambazo serikali imekuwa ikizitumia ni kama vile:- Moja, kuwapatia posho kubwa wakilishi na viongozi wa vyama pindi serikali na wawakilishi hawa wanapo kutana katika kujadili maslahi ya wafanyakazi ili kuwaziba mdomo. Pili, Kuwatishia kusitisha utaratibu wa kukusanya michango ya wanachama ila vyama vyenyewe vikusanye kwa njia wanaoijua wao. Tatu, kutofanya ukaguzi wa mara kwa mara katika vyama hivi vya wafanyakazi katika mapato, matumizi na miradi mbalimbali. Hii inasababisha vyama vya wafanyakazi kutofanya kazi ya kutetea wafanyakazi bali kutumia fedha na mali za vyama kwa manufaa binafsi.
c.       Kutumia vitisho na kauli za kutisha kudidimiza maslahi na haki za watumishi wa umma ikiwemo walimu. Viongozi wa serikali kama mawaziri na viongozi wengine waandamizi wa serikali wamekuwa wakitumia vitisho kwa wafanyakazi kama njia ya kuwanyamazisha wasidai maslahi yao.
3.      TAMKO KWA CHAMA CHA WALIMU-CWT NA SERIKALI YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA.
Sisi Walimu wa Mkoa wa Mbeya tunatoa siku 30 kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Na Chama Cha Walimu-CWT, Kuanzia leo Tarehe 03 August, 2013 hadi Tarehe 03 September, 2013 itekeleze yafuatayo:-
I.                   CHAMA CHA WALIMU-CWT
·         Kutoa taarifa ya fedha ya (Makusanyo ya kila mwezi) na mapato na matumizi ya chama hicho kwa walimu.
·         Kutoa taarifa ya wapi wamefikia kuhusu madai yetu dhidi ya serikali ya nyongeza ya mishahara kwa 100% na posho za mazingira magumu na kufundishia n.k, kwani ni muda sasa walimu tumechoka na ukimya wa CWT juu ya suala hilo.
·         Chama kisitishe makato haraka kwa walimu ambao si wanachama wa chama hicho.
·         Mkaguzi mkuu wa serikali (CAG) akague mwenendo wa miradi, mapato na matumizi ya Chama Cha Walimu-CWT na kutoa Taarifa kwa Walimu.
·         Kuboresha mfumo wa mawasiliano kutoka viongozi wajuu wa chama hadi walimu katika ngazi ya tawi.
II.                 SERIKALI YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
·         Serikali iweke sawa uwiano wa mishahara kisekta kulingana na viwango vya elimu kwa watumishi wa umma.
·         Serikali isitishe vitisho na matamko yenye vitisho kwa watumishi wa umma.
·         Serikali ipunguze kiwango cha kodi kubwa na kandamizi kwa watumishi wa umma, na itafute vyanzo vingine vya mapato
·         Serikali isizue watumishi kujiendeleza kwa sababu yoyote ile ili mradi wawewamekidhi vigezo vya kisheria vya kujiendeleza.
·         Serikali isitishe mpango wa kuligawa taifa kwa misingi ya maslahi binafsi, Kielimu, Kisekta na Nyadhifa.
·         Serikali ipandishe madaraja walimu waliojiendeleza kielimu ili kuwapa motisha.
Imetolewa na Walimu Wa Mkoa Wa Mbeya-Tarehe 03 August, 2013- Mkoani Mbeya.

0 comments:

Post a Comment