Thursday, November 15, 2012

 
Kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM-NEC) kimekutana katika Ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Chama, maarufu kama White House mjini Dodoma,l eo tarehe 14 Novemba 2012.

Kikao hicho kilijadili juu ya kuunda na kupitisha majina yaliyopendekezwa na Mwenyekiti wa Chama Mapinduzi Mheshimiwa Dkt Jakaya Mrisho Kikwete,  ya wajumbe wa Kamati Kuu ya Chama ya Taifa (CC) pamoja na uundaji wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa.

Mwenyekiti wa Chama kwa mujibu wa Kanuni na Katiba ya CCM, anayo fursa ya kuteua wajumbe kumi (10) wa Halmashauri kuu ya Taifa, ambapo  Mwenyekiti aliwateua wajumbe wanne (4) akabakiza nafasi nyingine sita (6).

Miongoni mwa wajumbe hao ni Mhe. Asha-Rose Migiro, Mhe. Zakhia Meghji, Mhe. Nape Nnauye na  Mhe. Abdulrahaman Kinana.

Baada ya uteuzi huo Mwenyekiti pia alipendekeza majina ya Wajumbe wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa, ambapo alipendekeza majina yafuatayo:

  1. Nafasi ya Katibu Mkuu, Abdulrahaman Kinana.
  2. Nafasi ya Naibu Katibu Mkuu Zanzibar,  Vuai Ali Vuai.
  3. Nafasi ya Naibu Katibu Mkuu Bara, Lameck Madelu Nchemba.
  4. Katibu wa Oganaizesheni, Mohamed Seif Khatib.
  5. Katibu wa Siasa na Mahusiano ya Kimataifa, Dkt. Asha-Rose Migiro.
  6. Katibu wa Uchumi na Fedha, Zakhia H. Meghji.

Baada ya mapendekezo hayo, Halmashauri Kuu ya Taifa ilipitisha majina hayo na kuyakubali kuwa hao waliopendekezwa ndiyo hasa wanaofaa kuwa wajumbe wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa.

Pia, Mwenyekiti akawashukuru wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa waliopita na pia kuwataka wajumbe wapya kuchapa kazi, na kuwataka kujenga mustakabali wa Chama, Uimara na Umadhubuti kwa kufanya kazi kwa kushirikiana na kusaidiana.

0 comments:

Post a Comment