Sunday, September 2, 2012

TUME ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania (TACAIDS) imeeleza kuwa rushwa ya ngono sehemu za utumishi wa umma ni changamoto mpya, inayochangia kukwamisha juhudi za kupunguza maambukizi mapya ya Ukimwi nchini.

Mwenyekiti Mtendaji wa Tacaids, Dk Fatma Mrisho, alisema hayo mwanzoni mwa wiki hii kwenye warsha ya siku mbili iliyoshirikisha watendaji wakuu kutoka Idara za Utumishi wa Umma.

Kutokana na kukithiri kwa aina hiyo ya rushwa katika utumishi wa umma, alitaka waajiri na watu wengine wenye tabia hizo kuacha na wazingatie haki, sheria na vigezo wanapohitaji kuajiri watumishi wapya.

Dkt. Mrisho alibainisha, kwamba Tanzania imefanikiwa kupunguza maambukizi ya UKIMWI tangu mwaka 2004 kutoka asilimia saba na kufikia asilimia 5.7. Akizungumzia mafanikio machache ya mkakati wa kupunguza maambukizi, alisema kuwa asilimia 94 ya Watanzania hawana maambukizi na hivyo ni vyema kila mmoja kuendelea kujikinga. Kutokana na mwelekeo huo, aliomba wananchi waendelee kuchukua hadhari za kujikinga ili wasiambukizwe.

Aliwasihi Watanzania wa jinsia zote kuacha kuwa na wapenzi wengi na kuendekeza rushwa ya ngono kwa vile tabia hizo zinachangia ongezeko la maambukizi mapya na kurudisha nyuma jitihada za Serikali juu ya kauli ya 'Tanzania bila Ukimwi inawezekana'.


0 comments:

Post a Comment