Monday, June 18, 2012

  Mabaunsa waunda umoja
Watu wanaodaiwa kuwa ni "mabaunsa" wameunda umoja wao na kuanza kukusanya ushuru kutoka kwa Wamachinga wanaopanga bidhaa zao katika kituo cha daladala cha Mwenge Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Mabaunsa hao wamedaiwa kufanya zoezi hilo huku wakishirikiana na baadhi ya watendaji wa Manispaa ya Kinondoni ambao wanawapa sehemu ya mapato wanayoyapata kutoka kwa wafanyabiashara hao.
Uchunguzi uliofanywa na NIPASHE umebaini kuwa "mabaunsa" hao ni sehemu ya wafanyakazi wa iliyokuwa kampuni iliyopewa tenda ya kukusanya ushuru wa daladala katika kituo hicho ambayo hata hivyo inadaiwa imemaliza muda wake wa kufanya kazi hiyo.
Watu hao wanadaiwa kukusanya kati ya Sh. 500,000 hadi 1,000,000 kutegemea wingi wa wafanyabishara kwa siku hiyo ambao wanapanga bidhaa zao kwenye meza na wengine wanaozishika mikononi kuanzia asubuhi hadi usiku.
Baadhi ya wafanyabishara hao ambao wanaendesha bishara zao kituoni hapo, waliliambia NIPASHE kuwa meza moja inalipiwa kati ya Sh. 5,000 hadi Sh. 7,000 kutegemea na ukubwa wa meza na kwamba fedha hizo zinatolewa kila siku.
Katika kituo hicho kuna zaidi ya meza 100 zilizozunguka eneo zima huku idadi ya wamachinga wanaotozwa ushuru bila ya kuwa na meza ikiwa haijulikani lakini fedha hizo zinadaiwa kuchukuliwa na mabaunsa bila kutoa stakabadhi.
Wamesema mtu anayekataa kulipa ushuru huo, anapigwa na watu ambao walidai wana miili mikubwa pamoja na kuwanyang'anya bidhaa zao zilizopo mezani na kwa wale wanaokuwa wamezishika mikononi.
Hata hivyo, walisema licha ya kulipa kiasi hicho cha fedha hawapewi stakabadhi na kwamba mfanyabiashara anayejaribu kudai anapigwa na kupelekwa kituo kidogo cha Polisi Mwenge.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Mwenge, Pascal Ng'itu alikiri kuwepo kwa hali hiyo na kusema kuwa watu hao wamekuwa wakifanya kazi hiyo kwa zaidi ya mwaka mmoja hadi sasa.
Alisema wafanyabiashara hao licha ya kuwa wapo katika eneo hilo kinyume cha sheria lakini kimeibuka kikundi cha watu wanaowalipisha ushuru huku mapato hayo yakiwa hayajulikani yanapelekwa wapi.
Alifafanua kuwa kwa muda wa mwaka mmoja, hakuna Mkandarasi anayejulikana kisheria ambaye amepewa kazi ya kukusanya mapato yatokanayo na ushuru wa magari ya daladala yanayotumia kituo hicho.
Ng'itu alisema kwamba kampuni iliyoshinda tenda ya kukusanya mapato katika kituo hicho, imenyimwa kazi hiyo na badala yake watu wasiojulikana ndiyo wanaoendelea kukusanya fedha zinazolipwa na daladala.

"Hiki kituo mimi kama mwenyekiti naona kuna uchafu mwingi na wa kutisha kwa sababu watu wanaokusanya ushuru haijulikani wanazipeleka wapi na ni kiasi gani kinachopatikana," alisema
Kwa mujibu wa taratibu za Manispaa ya Kinondoni, kampuni inayopewa tenda ya kukusanya ushuru inatakiwa kusimamia mapato yatokanayo na daladala, kuwaondoa wafanyabiashara ndogo ndogo, kukiweka kituo katika hali ya usafi pamoja na kuwaondoa wapiga debe.
Mkurugenzi mtendaji wa Manispaa ya Kinondoni, Fortunatus Fwema alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo alisema ameshtushwa huku akisema kwamba hajui kama kuna kikundi cha watu kinakusanya ushuru kutoka kwa wamachinga.

Alisema wamachinga hao wapo kituoni hapo kinyume cha utaratibu, lakini akasema pia watu wanawatoza ushuru wanahesabiwa kama wahalifu na kwamba watasakwa na Manispaa.
Alisema juhudi za kuwaondoa wamachinga pamoja na kumpata mkandarasi wa kukusanya ushuru zinafanyika na kwamba siku yoyote kuanzia sasa watavamia kituo hicho ili kuwatoa.
Alisema baada ya kumaliza kazi ya kuwaondoa wamachinga katika eneo la Ubungo na Tegeta kwa sasa zoezi hilo litahamia Mwenge muda wowote ili kuhakikisha kituo kinabaki wazi kwa ajili ya kuhudumia daladala.
Aliahidi kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini watendaji wa Manispaa wanaoshirikiana na kikundi hicho kukusanya ushuru kinyume cha sheria wala kufuata taratibu.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

0 comments:

Post a Comment