Monday, May 7, 2012

Baadhi ya vichwa vya habari ambayo ni wazi vinaumba picha ya namna fulani vichwani mwa jamii inayozisoma habari zenyewe na kufuatilia sakata la Lulu
Takriban mwezi mmoja sasa toka kufariki kwa msanii maarufu nchini, Steven Kanumba, huku msanii mwenzake Elizabeth Michael maarufu kwa jina la Lulu akiwa anaendelea kushikiliwa na vyombo vya dola kwa ajili ya uchunguzi kuhusiana na kifo hicho, vyombo vya habari vimeendelea kulivalia njuga suala hilo huku habari nyingi zikiwa zimejikita kwa mtuhumiwa Lulu.
Mengi yanazungumzwa kuhusu msanii huyo, kama ambavyo pichani vichwa vya habari vya baadhi ya magazeti vinajieleza. Hali hii kwa kiasi kikubwa imekuwa ikikinzana na taratibu za kisheria juu ya kuandika habari zenye kumhusu mtuhumiwa wa kosa fulani.
Bila kujali kilichomo au alichomaanisha mwandishi, ni wazi kuwa kwa ujumla wake, habari hizi zina athari ya namna yake kwa jamii inayosoma habari hizo na yenye kumfahamu Lulu, huku jamii hiyo ikiwa na hisia mchanganyiko kuhusu binti huyo.
Jambo lililo wazi ni kuwa, kwa kiasi fulani ni habari ambazo zimekuwa zikitengeneza picha fulani miongoni mwa jamii, picha ambayo kwa namna moja ama nyingine, kwa njia hasi au chanya, zinaweza kuathiri uchunguzi wa tukio hilo hali ambayo itakuwa na athari kubwa sana kwa upande wa Jamhuri unaoendesha uchunguzi wa suala hilo na Lulu mwenyewe kwa upande mwingine.
Ni katika mazingira haya basi, ambapo nimekuwa nikijiuliza kuwa, Je, tunamtendea haki Lulu kupitia maandishi yetu? Je, tunautendea haki upande unaofanya uchunguzi wa suala hili? Au maslahi yetu ya kibiashara ndio pekee tunayoyajali bila kuangalia upande wa pili?

0 comments:

Post a Comment