Tuesday, August 20, 2013

Picture
OCD Giresi Muroto akisalimiana na dereva wa gari ya Lema huku Wakili Mtui akishuhudia, nje ya Mahakama Kuu, Arusha.
Habari kwa mujibu wa blogu ya Noiz of Silence — Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha imeahirisha shauri la kesi inayomkabili Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Mhe. Godbless Lema (CHADEMA), kwa tuhuma za kuchochea vurugu katika Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA)  hadi Oktoba 1, 2013 ambapo mashahidi wa upande wa mashitaka wataanza kutoa ushahidi wao kwa siku mbili mfululizo.

Akitoa uamuzi huo mapema leo asubuhi Hakimu Devota Msofe alisema kwamba ameridhia ombi la Wakili wa Mhe. Lema aliyeomba shauri hilo liahirishwe kutokana na mteja wake kuwa mgonjwa. Hakimu Msofe 
aliwataka mashahidi wote kama walivyohuduria leo kufika Mahakamani hapo siku ya Jumanne na Jumatano ya Oktoba 1 na 2 kwa ajili ya kuanza kutoa ushahidi wao, zoezi ambalo lilipangwa kuanza leo kama kuningekuwa na udhuru wa kuahirisha shauri hilo.

Mashahidi wa upande wa Jamhuri waliofika Mahakamani hapo ni pamoja na OCD wa Wilaya ya Arusha Mjini, Giresi Muroto na Mlezi wa Wananfunzi chuoni hapo Bw John Joseph Nanyaro. Wengine ni Inspekta wa Polisi Bernad Nyambalya, Makamu Mkuu wa Chuo cha IAA Bw Faraj Kasidi na Jane Chibuga.

Awali Wakili Kimomongoro anayemwakilisha Lema wakisaidiana na Wakili, Humrefy Mtui aliwasilisha ombi la kuiomba mahakama iahirishe shauri hilo hadi tarehe nyingine kwa kile alichoeleza kuwa ni kutokana na Mhe. Lema kuwa katika hali ya kuumwa na kwamba ni jana tu aliruhusiwa kutoka hospitali ya AICC alikokuwa amelazwa tangia Agosti 14 akiendelea kutumikia siku 10 alizopewa na daktari za mapumziko ya kitandani.

Wakili Kimomongoro alimkabidhi mwanasheria wa Jamhuri nakala ya “Discharge Summary” kutoka hospitali ya AICC nae akaipitia na kuridhia shauri hilo kuahirishwa kutokana na sababu hiyo ya ugonjwa.

Source: http://www.wavuti.com/4/post/2013/08/kesi-ya-uchochezi-chuoni-arusha-yaahirishwa-kutokana-na-lema-kuwa-mgonjwa.html#ixzz2cXlG5ybB

0 comments:

Post a Comment