Wednesday, October 10, 2012

Wakati Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, akikituhumu Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwamba kinanuka rushwa, kada mwingine wa chama hicho ameandika kitabu kinachoeleza namna rushwa ilivyoota mizizi nchini kuanzia kwenye siasa, ofisi za umma na jamii kwa ujumla.

Kitabu hicho kimeandikwa na aliyekuwa Kamishna wa Madini na Mbunge wa Igunga wa CCM, Dk. Peter Kafumu, na kuandikiwa dibaji na Rais mstaafu, Benjamin Mkapa.

Kitabu hicho kinachoitwa “Sauti Inayolia-Tafakuri Binafsi” (a Crying Voice-personal reflections), pamoja na mambo mengine, kinaeleza kwamba jamii ya Tanzania kwa sasa imekithiri kwa rushwa kuliko wakati mwingine wowote; kuanzia kwa watumishi waandamizi serikalini, wadogo na wanasiasa.

Katika kitabu hicho, Dk. Kafumu ambaye alishinda ubunge katika uchaguzi mdogo wa mwaka jana kwa tiketi ya CCM katika Jimbo la Igunga, mkoani Tabora na baadaye Mahakama Kuu ilitengua ushindi wake, anaeleza kuwa baadhi ya wanasiasa wanapata nyadhifa mbalimbali kwenye vyama na hata ubunge kwa kutoa rushwa, “Maamuzi ya wapigakura na mamlaka za uteuzi yanashawishiwa na rushwa; mameneja katika taasisi na idara za serikali wanakula rushwa ili wawe matajiri,” anaeleza.

Kitabu hicho kinaeleza zaidi kwamba asilimia kubwa ya watu wa kawaida wapo tayari kupokea rushwa ili kupata ama kutoa huduma kwa umma kama afya au elimu ambazo ni bure, jambo linalolazimisha wananchi kutoa kitu kidogo ili kuokoa maisha yao, “Wengine wanatoa ama kupokea rushwa kwa sababu wanasukumwa na tamaa ya kutajirika au kupata nafasi ya kisiasa au mamlaka kwa umma,” anaeleza Dk. Kafumu katika kitabu hicho.

Anaeleza kuwa rushwa imeota mizizi kwa namna isivyoelezeka na kwamba ni janga wakati wa sasa ambalo ni sawa na jinamizi linaloisumbua jamii.

Anaeleza kuwa rushwa hivi sasa ndiyo inayoshamirisha hali mbaya ya umasikini nchini na katika nchi nyingine za dunia ya tatu.

Hata hivyo, anaeleza kuwa hofu ya kifo baada ya kustaafu inachangia kuongezeka kwa rushwa nchini kwa sababu watumishi wa umma na wanasiasa wanajiingiza kwenye vitendo vya rushwa kama njia ya kujipatia utajiri kwa manufaa ya baadaye.

Anaeleza kuwa rushwa kubwa iliyofanywa na watumishi wa umma na wanasiasa inakejeli rasilimali za taifa ambazo zingeweza kutumiwa vizuri kukuza uchumi wa nchi na kuondoa umaskini.

Anasema rushwa kubwa zimesababisha ‘kurundika’ utajiri mikononi mwa watu wachache huku ikiacha taifa likiwa duni na mamilioni ya wananchi wakielea kwenye umaskini uliokithiri.

Dk. Kafumu anaeleza kwamba: "Rushwa kubwa na ndogo zimeiandama jamii kiasi kwamba kila siku tunakutana, kuzungumza, kuishi na kufanya kazi na watu ambao wanaonekana ni watu wasafi, lakini ndiyo washirika vitendo vya rushwa katika hali ya juu kabisa.”

Anafafanua kuwa hali hiyo imeharibu mitazamo ya watu kiasi cha kuona kuwa kutoshiriki vitendo vya rushwa au kuwa mwaminifu hailipi; kwamba kuishi kwa uaminifu katika jamii iliyokithiri kwa rushwa ni sawa na tone la damu ya samaki aliyejeruhiwa baharini.

“Rushwa sasa ni mizizi mikubwa katika jamii ya Watanzania, ni mwiba katika taifa maskini linalopambana kuendeleza watu wake,” anasema.

Anaeleza kuwa rushwa inaua wanyonge wakiwamo wagonjwa, masikini na wajane ambao wanakosa matibabu, elimu na huduma nyingine muhimu kwa sababu hawana kitu kidogo cha kuhonga.

Kitabu hicho kina sura tano, ikianza na Kumuienzi Kiongozi Jabali (Cherishing Great Leader); Rushwa; Sayansi, Dini na Jamii; Mabadiliko ya Tabia Nchi Duniani na Asili na Maendeleo ya Kiuchumi.

---
Habari hii ni kwa mujibu wa gazeti la Nipashe

0 comments:

Post a Comment