Sunday, June 17, 2012

WAKATI Chama Cha Wananchi (CUF), kikiwaagiza wabunge wake kuipinga bajeti ya serikali, serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) sasa imelazimika kuwatisha wabunge wake, ili waipitishe.
Hatua hiyo ya CUF inaelezwa imekitikisa zaidi chama tawala na serikali yake ambayo sasa huenda italazimika kuifanyia mabadiliko makubwa bajeti iliyosomwa Juni 14 mwaka huu ambayo imefikia sh trilioni 15 kutoka trilioni 13.5 za mwaka 2011/2012.
Wachambuzi wa masuala ya siasa na uchumi wameweka wazi kuwa, kama serikali haitokubali kubadilisha na kuongeza fedha kwenye miradi ya maendeleo, itegemee kukwama kwa bajeti.

CCM kipo katika wakati mgumu hivi sasa kwa sababu tayari wabunge wake wametangaza kuipinga, huku wengine wakiweka wazi kuwa ni afadhali kufukuzwa chama kuliko kupitisha mambo yasiyo na masilahi kwa wananchi waliowachagua.
Matokeo ya kupingwa kwa bajeti hiyo na vyama vya upinzani, wachumi na wananchi wa kawaida, yamepata uzito mkubwa kufuatia kitendo cha kujitokeza hadharani kwa baadhi ya wabunge wa CCM ambao wameanika kasoro kubwa zilizomo, huku wakiishutumu serikali kwa kuandaa bajeti iliyowasahau wananchi wa kipato cha chini.

Kujitokeza Alhamisi wiki hii, kwa Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM) ambaye alifichua kukiukwa kwa makubaliano ya kuifanyia marekebisho muhimu bajeti, na kufikia hatua ya kuapa kuwa ataipinga kwa nguvu zote hata kama itamlazimu kufukuzwa ndani ya chama hicho.
Mpina alisema hawezi kuendelea kuwa mbunge wa CCM kwa hali hiyo, na kwamba ni aibu kwake kuiunga mkono bajeti isiyolenga kumkomboa mwananchi, huku ikiruhusu fedha nyingi kutumika katika mambo yasiyo ya msingi.

Mbunge huyo ambaye amekuwa akitumia vielelezo kuweka uzito madai hayo, anatoa mfano wa jinsi Wizara ya Nishati na Madini ilivyojitengea kiasi cha zaidi ya sh milioni 567, kwa mawasiliano tu, badala ya sh milioni 72 ilizotumia mwaka jana.
Aliongeza kuwa, wizara hiyo imejitengea pia sh bilioni 2 zitakazotumiwa na kitengo cha mawasiliano na utawala, wakati mwaka jana kilitumia sh milioni 53.87.
Wizara ya Fedha nayo inadaiwa kujitengea sh bilioni 1.456 kwa ajili ya safari za ndani na nje ya nchi, wakati mwaka jana ilitumia sh milioni 815.

Hata hivyo, habari za kuaminika zimedai kuwa, Mpina hayuko peke yake, bali kuna kundi kubwa la wabunge wa CCM nyuma yake, ambao wanamuunga mkono na wameapa kuikwamisha bajeti, na ikishindana watatumia njia ya kuzigomea na kuzikataa bajeti za wizara.
Habari zinadai kuwa, tayari uongozi wa juu wa CCM umeanza kuwafuatilia kwa siri wabunge wake wanaoonekana kuwa wabishi, ili kujua wanapata wapi ujasiri huo, huku kukiwa na hofu kuwa wanatumiwa na kundi moja la viongozi ndani ya chama hicho, na wengine wakiwa mawakala wa vyama vya upinzani.
Katika kile kilichoonekana kukabiliana na tishio hilo, juzi wabunge wa CCM waliitwa chini ya uenyekiti wa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na kujifungia tangu saa 5:00 asubuhi hadi 12:30 jioni, ambapo inadaiwa walilazimika kuipitia kikamilifu bajeti hiyo.

Katika kikao hicho, inadaiwa kuwa baadhi ya wabunge waliweka wazi msimamo wao wa kuikataa bajeti hiyo, wakikosoa vifungu vingi na wengine wakienda mbali zaidi wakidai kuwa serikali ilikuwa imewasaliti wabunge na wananchi, kwa kutoa fedha kidogo katika shughuli za maendeleo.
Inadaiwa wabunge wengi walisema wataiunga mkono na kuipitisha, ikiwa tu serikali itakubali kuifumua katika baadhi ya maeneo mengi na kupeleka fedha nyingi katika shughuli za maendeleo.
Kikao hicho kilikuwa ni cha pili ambapo katika kikao cha kwanza, wabunge wa CCM walitishwa kuchukuliwa hatua za kinidhamu, ikiwemo kusimamishwa ama kuvuliwa uanachama, ikiwa wataendelea na msimamo wao wa kupinga bajeti na kuwashambulia watendaji wa serikali.

Mashambulio hayo yalimwelemea zaidi Mbunge wa Mwibara, Kange Lugola, ambaye mapema wiki hii, alisimama bungeni kuomba mwongozo wa Spika, akimtaka aliyekuwa Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo afute ama kuthibitisha kauli yake kuwa wabunge wa Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma (POAC) ilikuwa imehongwa.

Kange hata hivyo, alijaribu kujitetea huku akidai kutukanwa matusi ya nguoni na Mkulo, jambo lililozidi kuchafua hali ya hewa ndani ya kikao hicho, huku waziri huyo wa zamani aliapa kupambana na yeyote anayeonekana kumsakama.
Habari zinasema kuwa, kama moja ya mbinu ya kuzima misimamo mikali ya wabunge, Waziri wa Nchi, Utawala Bora, George Mkuchika, alisema sasa atamshughulikia kikamilifu mbunge yeyote wa CCM atakayethubutu kukwamisha mipango ya chama chao na serikali yake kwa kuwa anao uwezo huo.

Wabunge wa CCM ambao mara kwa mara wamekuwa wakielezwa kutokubaliana na uamuzi wa serikali ya chama chao, juzi walikwepa kuhudhuria kikao cha wabunge wa chama hicho kwa lengo la kukwepa kufungwa midomo.
Hoja ya wabunge hao ni kwamba wanataka kuisulubu serikali yao bungeni, ambako ndiko uwanja wao wa kujidai badala ya kuijadili kwenye kikao cha chama.

CUF yaigomea bajeti
Chama cha Wananchi (CUF), jana kiliwaagiza wabunge wake kuipinga bajeti hiyo, kwa kile walichodai ni ya kibangaizaji sambamba na kuwa imeandaliwa kwa lengo la kuwadanganya wananchi.
Agizo hilo limetangazwa jana na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, mbele ya wabunge wa chama hicho na waandishi wa habari, alipokutana nao mjini hapa, akisema hawawezi kuunga mkono bajeti aliyodai imejaa ubabaishaji na ni ya kisanii.
Lipumba alisema hawawezi kuunga mkono bajeti isiyowakwamua kabwela wa Tanzania kutoka katika lindi la umasikini, na kuongeza kuwa hali ya wananchi ni mbaya na mfumuko wa bei umeongezeka kutoka asilimia 10.9 mwaka jana hadi asilimia 18.

Apongeza utawala wa Mkapa
Profesa Lipumba aliushutumu uongozi wa Rais Jakaya Kikwete kwa kuzembea katika nidhamu ya matumizi ya fedha za umma, huku akimmwagia sifa Rais wa zamani, Benjamin Mkapa.
“Tumefikishwa hapa na serikali hii isiyokuwa na nidhamu ya matumizi ya fedha. Wakati wa utawala wa Mkapa, kulikuwa na udhibiti mkubwa wa fedha, na alibana kiasi kwamba, hata waziri hakuruhusiwa kusafiri bila kibali chake.

“Hali ya sasa ni ovyo, na umekuwa utawala wa Gezaulole, kila mtu anajifanyia atakalo,” alisema Lipumba.
Kiongozi huyo ambaye ni mtaalamu wa uchumi, alisema kumekuwa na ongezeko kubwa la deni la taifa, matumizi mabaya ya fedha, na ahadi hewa za kukamilisha mradi wa umeme wa megawati 60 ambao serikali imekuwa ikiutolea maelezo kila mwaka.
Alifichua kuwa, serikali imemlipa mtaalamu wa kigeni dola milioni 40, kutokana na mkopo wa dola milioni 400 kwa masharti ya kibiashara, na ikaficha kuliweka jambo hilo katika kumbukumbu za vitabu.
“Awali tulikopa dola milioni 400 na gharama za mshauri ilikuwa dola milioni 40 kabla ya riba. Hapa haikuelezwa gharama za kukopa, wala haikusema, tumelijua hili baada ya kuona ripoti za Benki ya Dunia,” alisema Lipumba.

CHADEMA kuitikisa zaidi
Wakati hali ikionekana kuiendea kombo Serikali ya CCM, macho na masikio ya watu wengi kesho yataelekezwa katika hotuba ya kambi rasmi ya upinzani inayoongozwa na Mwenyekiti wa CHADEMA, ambaye pia ni Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe.
Tayari kambi hiyo imeshaweka wazi kuwa bajeti hii haijalenga kumkomboa mwananchi, hivyo katika mazingira ya kawaida mjadala wke utakuwa mkali zaidi CHADEMA ambayo mara kwa mara imekuwa ikiwapa shida CCM kwenye mijadala mbalimbali, sasa itaipasua zaidi bajeti kwa kuwa CUF na baadhi ya wabunge wa chama tawala wameonekana kuangalia zaidi athari za bajeti hiyo kwa wananchi.
Juzi, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, alisema hotuba ya bajeti imedhihirisha kuwa serikali iko taabani na haiwezi tena kuwa na ujasiri wa kuongoza nchi.

Dk. Slaa alisema hatua ya serikali kutenga asilimia 70 ya fedha kwa ajili ya matumizi ya kawaida na mengine yasiyokuwa ya lazima, huku ikibakiza asilimia 30 tu katika matumizi ya maendeleo ambazo zaidi ya nusu yake zitatokana na misaada na mikopo ya kigeni, ni ushahidi tosha kuwa serikali haijali shida za watu.
Alisikitishwa na kuongezeka kwa deni la taifa, akidai kuwa halimnufaishi hata kidogo mwananchi wa kawaida kwa kuwa zinaishia katika mikono ya wajanja.
Habari  na Charles Misango, Dodoma

0 comments:

Post a Comment