Friday, October 19, 2012

Mfanyakazi wa ndani, Angel Lema (22) amechomwa kisu kwa tuhuma za kuwa na uhusiano wa kimapenzi na baba mwenye nyumba anakofanya kazi.

Angel anayefanya kazi za ndani katika kijiji cha Leganga wilayani Arumeru mkoani Arusha, inadaiwa alifanyiwa unyama huo na mama mwenye nyumba baada ya kumhisi ‘kutembea’ na mumewe.

Akizungumzia tukio hilo jana, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru, Dkt. Aziz Msuya, alithibitisha kumpokea msichana huyo akiwa na hali mbaya, kutokana na jeraha tumboni Oktoba 8. Dkt. Msuya alidai baada ya kufanyiwa uchunguzi, ilibainika alichomwa kisu tumboni na mwajiri wake.

“Lakini binti huyu tulipomhoji, kwanza alikataa na kudai kujichoma mwenyewe, ila baadaye ilibainika alichomwa na mama mwenye nyumba kwa hisia za kufanya mapenzi na mumewe na kumeonya asimtaje kuwa ndiye amemchoma kisu,” alidai.

Dkt. Msuya alisema kutokana na jeraha kuwa kubwa, walihofia usalama wa utumbo wake na kulazimika kumfanyia upasuaji wa tumbo ili kuangalia usalama zaidi ndani, “Tulipomfanyia upasuaji tuligundua hajaathirika utumbo na ulikuwa salama, tukamshona,” alisema Dkt. Msuya na kuongeza: “Lakini cha ajabu kidonda kikiwa kibichi, msichana huyo alitoroshwa usiku Oktoba 14, kitendo kilichotushangaza,” alisema Dkt. Msuya.

Alisema baada ya kugundua hilo, walitoa taarifa Polisi, ili wachunguze tukio hilo ili kuokoa maisha ya msichana huyo. Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Liberatus Sabas baada ya kupigiwa simu na gazeti hili, kuuliziwa tukio hilo, alisema hana taarifa, “Mimi sina taarifa, lakini tukio hilo linaweza kuwapo… kwa kuwa niko mbali huku Moshi kwenye maziko ya Kamanda Barlow (Liberatus), bado sijapata muda wa kufuatilia taarifa za huko na kupata habari zaidi, lakini pia huku mawasiliano yanasumbua sana,” alisema.

Kamanda Sabas aliahidi kulifuatilia suala hilo mara atakapopata nafasi na kutoa taarifa.

---
Habari imeandikwa na John Mhala, HabariLeo, Arusha

0 comments:

Post a Comment